Sunday, May 30, 2010

Magari ya TOT yakamatwa Dar



Na Peter Mwenda

MAGARI ya Kikundi cha Uhamasishaji cha Chama Cha Mapinduzi (CCM) cha Tanzania One Theatre (TOT) yamekamatwa na Kampuni ya Udalali ya Majembe Auction Mart baada ya kushindwa kulipa deni la Benki ya Wananchi wa Dar es Salaam (DCB).

Habari zilizopatikana kutoka katika yadi ya Kampuni Majembe iliyoko Mwenge zimesema magari hayo yamekamatwa baada ya kushindwa kulipa sh milioni 30 za DCB.

Mkurugenzi Mtendaji wa DCB, Bw. Edmund Mkwawa alithibitisha jana kuwapa kazi Majembe ya kukamata magari ya TOT baada ya kushindwa kulipa deni, lakini hakuwa tayari kutaja kiwango cha deni hilo.

"Ni kweli tunawadai, tumekuwa tukiwataka walipe deni lao kwa muda mrefu lakini hawatimizi ahadi, kwa mara ya mwisho tulipawa mwezi mmoja lakini hawakufanya hivyo," alisema Bw. Mkwawa.

Hata Mkurugenzi wa Kampuni ya Majembe, Bw. Seth Mwamoto alipoulizwa kiasi gani ambacho TOT inadaiwa alisema waulizwe DCB.

Mkurugenzi Mtendaji wa TOT, Kapteni John Komba alipoulizwa alikiri TOT kudaiwa na benki hiyo, na kuwa kiwango kilichosalia sasa ni sh. milioni 30 ambazo alisema zitalipwa mwezi ujao.

"Sisi si wa kwanza kudaiwa wala magari kukamatwa, hakuna cha ajabu, tutalipa deni hilo, nimepokea simu nyingi wakitaka kujua habari hizi, wabaya wangu wamefurahi sana, lakini kitu gani cha ajabu kama serikali yenyewe inadaiwa, sembuse TOT?alisema kapteni Komba.

Kikundi cha TOT ni mhimili wa kuhamasisha wapiga kura wa CCM wakati wa kampeni na kinategemwa katikja Uchaguzi Mkuu wa Oktoba mwaka huu.

No comments:

Post a Comment